Showing posts with label Habari. Show all posts
Showing posts with label Habari. Show all posts

Friday, May 31, 2019

ATCL yamvuruga Nape, ahoji kucheleweshwa kwa ndege

ATCL yamvuruga Nape, ahoji kucheleweshwa kwa ndege

Serikali yakanusha kuwalazimisha wafanyakazi wake kuwa na laini ya TTCL


Msemaji wa Serikali, Dk Hassan Abbas amesema hakuna agizo la Serikali linalolazimisha mfanyakazi wa Serikali kuwa na laini ya TTCL isipokuwa viongozi wanaowekewa vocha za Serikali kwamba ni muhimu kuwa na laini hizo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo amesema taarifa inayosambaa kwenye mitandao kuhusu hilo ni ya upotoshaji na kuwataka wananchi kuipuuza.

Wednesday, May 29, 2019

Rais Magufuli ataka Jumuiya za Kimataifa kuondoa vikwazo dhidi ya Zimbabwe

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amempongeza Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe Emmerson Mnangagwa kwa hatua madhubuti za kufanya mageuzi ya kiuchumi katika nchi hiyo na ametoa wito kwa Jumuiya ya Kimataifa kuondoa vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Zimbabwe.

Rais Magufuli amesema hayo wakati akitoa hotuba katika Dhifa ya Kitaifa iliyoandaliwa na Rais Mnangagwa kwa heshima yake na kufanyika Ikulu Jijini Harare.

Rais Magufuli amesema katika kipindi kifupi cha tangu Rais Mnangagwa aingie madarakani hali ya uchumi imeanza kuimarika ambapo kwa sasa uchumi wa Zimbabwe unakua kwa wastani wa asilimia 3.5, mwaka ujao unatarajiwa kukua kwa wastani wa asilimia 4.2 na mwaka unaofuata kuongeza hadi wastani wa asilimi 4.4.

Kufuatia hali hiyo ameisihi Jumuiya ya Kimataifa kuondoa vikwazo mbalimbali vilivyowekwa dhidi ya Zimbabwe kwa kuwa vikwazo hivyo vinawaumiza wananchi wa Zimbabwe wakiwemo watoto na wanawake.

Katika hotuba hiyo, Rais Magufuli kwa mara nyingine amewapa pole Rais na wananchi wote wa Zimbabwe kwa kupoteza watu takribani 400 waliofariki dunia katika mafuriko yaliyosababishwa na Kimbunga Idai kilichoikumba Zimbabwe Machi 2019. Amesema Watanzania wanaungana na ndugu zao Wazimbabwe katika majonzi ya kuondokewa na jamaa zao na wanawaombea kwa Mwenyezi Mungu aziweke roho zao mahali pema peponi, Amina.

Kuhusu uhusiano wa Tanzania na Zimbabwe ulioasisiwa na Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere na Mzee Robert Mugabe, Rais Magufuli amesema Tanzania inatambua na inathamini uhusiano huu wa kihistoria na kidugu na amebainisha kuwa jukumu lililopo sasa ni kuelekeza nguvu nyingi zaidi katika uhusiano na ushirikiano wa kiuchumi utakaoziwezesha Tanzania na Zimbabwe kuongeza biashara na uwekezaji.

Rais Magufuli amebainisha kuwa katika mazungumzo yake ya faragha na Rais Mnangagwa leo mchana wamekubaliana kusimamia ipasavyo makubaliano yaliyopo katika Kamati ya Pamoja ya Kudumu (Joint Permanent Commission – JPC) kwa manufaa ya nchi zote mbili.

“Rais Mnangagwa ujio wangu hapa Zimbabwe ni kuthibitisha kuwa urafiki wetu bado upo imara na sisi Tanzania tumejipanga kuuimarisha zaidi, tunataka tufanye biashara zaidi na nyinyi ndugu zetu wa Zimbabwe ili tukuze uchumi wa nchi zetu na kuongeza kipato cha wananchi wetu” amesisitiza Rais Magufuli.

Kwa upande wake, Rais Mnangagwa amemshukuru Rais Magufuli kwa kukubali mwaliko wake, na amemthibitishia kuwa yeye na wananchi wa Zimbabwe wanatambua kuwa Watanzania ni ndugu zao waliojitolea kwa dhati katika ukombozi wao wakiongozwa na dhamira ya dhati ya Hayati Mwl. Nyerere.

Amemshukuru Rais Magufuli kwa kuwa kiongozi wa kwanza katika nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kutoa msaada wa chakula, dawa na vifaa vya kujihifadhi wakati Zimbabwe alipokumbwa na mafuriko yaliyosababishwa na Kimbunga Idai mwezi Machi 2019.

Rais Mnangagwa amesema msaada huo uliwagusa Wazimbabwe wengi na kuwakumbusha umuhimu wa kuchukua tahadhari dhidi ya majanga na mabadiliko ya tabia nchi.

Amesisitiza kuwa daima Zimbabwe itabaki kuwa rafiki na ndugu wa kweli wa Tanzania na hivyo amemhakikishia Rais Magufuli kuwa nchi hiyo ipo tayari kukuza zaidi ushirikiano wa kiuchumi kwa kuongeza biashara na uwekezaji pamoja na kushirikiana katika usafiri wa anga.

Amemshukuru Rais Magufuli kwa kumpa mbinu mbalimbali za kiuongozi ikiwemo kuondoa watumishi hewa ambao wamekuwa mzigo mkubwa kwa Serikali na ameahidi kudumisha ushirikiano kati ya chama chake ZANU-PF na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Makonda atangaza vita na Wamachinga wasio na vitambulisho Dar


Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda amesema kuanzia June 3 mwaka 2019 ni marufuku kwa Wamachinga wote wasio na vitambulisho kufanya biashara katika maeneo yote jijini Dar.

Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Mei 29, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari kuhusu mwitikio wa wafanyabiashara kuchukua vitambulisho hivyo vilivyotolewa na Rais John Magufuli kwa wakuu wote wa Mikoa nchini.

Makonda amesema Jiji hilo lilipatiwa vitambulisho 175,000 lakini wapo ambao hawajachukua hadi sasa.

Amesema kuwa atafanya msako mkali kuwatafuta wamachinga wote wasio na vitambulisho hivyo

NACTE Yasitisha Udahili Kozi Ya Hudumu Ya Afya Ngazi Ya Jamii Kwa Mwaka Wa Masomo 2019/2020


Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi(NACTE)limetangaza kusitisha udahili wa wanafunzi wapya wa program ya Huduma ya Afya Ngazi ya Jamii(Community Health) kwa mwaka wa masomo 2019/2020 hadi hapo itakapotangaza tena.

Akizungumza mbele ya wanahabari Jijini Dodoma  janas Mkurugenzi wa uzingativu, ufuatiliaji na Tathmini wa NACTE Jofrey Oleke, amesema maombi ya udahili kwa waombaji wapya wa Astashahada na Stashahada kwa mwaka wa masomo 2019/2020, umesitishwa hadi hapo baraza litakapotangaza maamuzi mengine.

Kufutwa kwa udahili huo kumetokana na maelekezo yaliyotolewa na Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto kwamba kwa mwaka huu wa masomo hakutakuwa na kozi hizo.

Kuhusu kusitishwa kwa udahili, amesema baraza limepokea maagizo kutoka wizara ya afya ambao ndio wanaosimamia kozi zote za afya, kuwa katika mwaka huu wa masoma hakutakuwa na udahili katika ngazi hiyo afya ya jamii nasi tunatekeleza.

“Baraza linavitaarifu vyuo na umma kwamba udahili wa wanafunzi katika programu ya Huduma ya afya Ngazi ya Jamii umesitishwa hadi hapo itakapotangazwa tena”,amesema.

Pia baraza limetangaza kufunguliwa kwa udahili mpya kwa ngazi za Astashahada na stashahada kwa kozi zote isipokuwa kwa kozi za ualimu na utaendelea mpaka tarehe 2 mwezi wa tisa mwaka huu kwa vyuo vyote vinavyotoa mafunzo katika ngazi hizo.

Amefafanua kuwa kwa waombaji wa programu za Afya katika vyuo vya Serikali watatakiwa ama kuomba moja kwa moja kupitia vyuoni ambapo vyuo vitasawasajili kupitia baraza la chuo au wanaweza kuomba kupitia tovuti ya Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (www.nacte.go.tz) kubonyeza kwenye ‘apply online'(SAVS).

Kuhusu waombaji wa programu za Afya kwenye vyuo visivyo vya Serikali na waombaji wa programu nyingine zote wanatakiwa kuomba moja kwa moja kwenye vyuo husika.

“Hivyo vyuo vitapokea maombi na kufanya uchaguzi wa wanafunzi wenye sifa na kisha wawasilishe NACTE majina ya waliochaguliwa kwa ajili ya uhakiki kabla ya kuyatangaza, vyuo vinaelekezwa kuzingatia utaratibu wa udahili kama ulivyotolewa na baraza katika mwaka wa masomo 2019/2020,”amesema.

Amewataka wahitimu wote wa Elimu ya Sekondari na vyuo wenye sifa za kujiunga na kozi za Astashahada na Stashahada, kufanya maombi kwa umakini ili kuweza kupata nafasi ya kujiunga programu wanazozipenda na ambazo wanatimiza vigezo/sifa za kujiunga nazo kwa mwaka 2019/2020.

Pia baraza limewashauri waombaji na wazazi kuhakikisha kuwa wanaomba kwenye vyuo vinavyokidhi ubora ambavyo vimeorodheshwa kwenye kitabu cha mwongozo wa udahili kwa mwaka wa masomo mwaka 2019/2020 .